Athari ya Rasimu za Breili katika Usimilishaji wa Ishara Za Isimu
Ikisiri
Utafiti huu ulinuia kuchanganua usimilishaji wa ishara za isimu katika breili ya Kiswahili. Uchanganuzi huu ulitiwa hamasa na mambo matano muhimu. Kwanza, breili ndio njia ya pekee ya uandishi ambayo watu wasioona hutumia katika mawasiliano na usomi wao. Vilevile, kutokuwepo kwa kipengele muhimu cha matamshi katika kamusi za breili na vitabu vya sarufi hasa vya sekondari. Jambo jingine ni kwamba, wanafunzi wanaotumia breili hupewa maswali mbadala wakati wanapotahiniwa katika maeneo ya fonolojia, mofolojia na hata katika uchanganuzi wa sentensi. Aidha, kutokuwepo kwa ishara bainifu za isimu katika maandishi ya breili ya Kiswahili. Kichocheo cha mwisho, praima mbili za breili ya Kiswahili: ya 1978 na 1995 zinazotumiwa Afrika Mashariki hazina ishara za kiisimu. Utafiti huu ulikusudia kujibu maswali yafuatayo: changamoto zipi zinazozuia usimilishaji wa ishara za kiisimu katika breili ya Kiswahili? Rasimu za Kiingereza na Kiswahili huathiriana kwa njia zipi? Ukosefu wa ishara za isimu katika breili huathiri ufundishaji wa isimu kwa njia gani? Na mwisho, mikato ya Kiswahili na ya Kiingereza inayotumia nukta zinazofanana huathiri uchapishaji wa vitabu vya isimu kwa njia zipi? Utafiti huu ulilenga kutimiza malengo yafuatayo – kwanza, kubainisha na kutatua changamoto zinazozuia usimilishaji wa ishara za isimu katika breili ya Kiswahili. Pili, Kuchanganua rasimu ya Kiingereza na ya Kiswahili. Aidha, kuchunguza athari ya ukosefu wa ishara hizi katika ufundishaji wa isimu. Mwisho, kutathmini athari ya matumizi ya mikato inayotumia nukta zinazofanana katika uchapishaji wa vitabu vya isimu. Makala haya yatashughulikia lengo la kwanza. Mbinu za utafiti zifuatazo ndizo zilizotumiwa kukusanya data; uchunzaji, hojaji na mahojiano. Utafiti huu ulichanganua usimilishaji wa ishara hizi kwa kuzingatia nadharia ya usomaji na uandishi wa breili iliyoasisiwa na Kizuka na Fuji (2005). Mtafiti aligundua kuwa uchache wa nukta nundu umesababisha uradidi mwingi wa matumizi ya nukta nundu hizi. Uradidi huu umechangia kuwepo kwa utata wa kimaana katika fonolojia na sintaksia ya Kiswahili, vikwazo vya ufundishaji wa isimu miongoni mwa wanafunzi wasioona, makosa katika vitabu vya sarufi hasa kidato cha kwanza na kidato cha pili na changamoto zinazotinga usimilishaji wa ishara za kiisimu katika Breili. Utafiti huu utawafaidi wanafunzi wanaotumia breili na walimu na wahadhiri wanaofunza isimu
Upakuaji
Marejeleo
Dooley, D. (1984). Social Research Methods. Englewood Cliffs, N.J.: Prentice Hall inc.
Fanike, J. (1984). Exceptional Child.Oxford University Press.
Ipara, I., Burudi, J.,, & Wakio, N. (2010). Upeo wa sarufi kwa shule za sekondari. Oxford University Press.
Kothari, C. (1985). Research Methodology: Methods and Techniques.New Age International Publishers.
Mvati, M., Maina, R., na Kanuri, J. (2014). Miale ya Sarufi. The fransiscan Kolbe Press.
Prima (1978). Kiswahili Braille: KIB.
Prima (1993). Kiswahili Braille: KIB.
Travers, R. M. W. (1978). An introduction to educational research.Collier-Macmillan.
D’Andrea, F. M., Wormsley, D. P., & Savaiano, M. E. (2014). Unified English Braille in the United States: A research agenda for transition and instruction. International review of research in developmental disabilities, 46, 145-175.
Copyright (c) 2024 Daniel Mburu Mwangi, PhD
This work is licensed under a Creative Commons Attribution 4.0 International License.